September 2020



VINARA wa Ligi Kuu Bara, KMC FC mchana huu inatimka zao kwenda mkoani Shinyanga kwa ajili ya mchezo wao watatu katika ligi hiyo dhidi ya wenyeji wao Mwadui FC.

Mchezo huo utakaochezwa Jumatatu kwenye Uwanja wa Mwadui Complex, mjini Mwadui ni wa kwanza kwa KMC ugenini na wa tatu katika ligi hiyo.

Katika mechi mbili za awali, KMC iliinyoa Mbeya City kwa mabao 4-0 kisha kuichapa Tanzania Prisons kwa mabao 2-1 na kuongoza msimamo kwa faida ya uwiano mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa dhidi ya Azam, Biashara Utd na Dodoma Jiji wanaolingana nao pointi kila moja ikiwa na sita baada ya mechi mbili mbili.

Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa KMC, Christina Mwagala kikosi hicho kitaondoka na wachezaji 22 , huku sita wakiwachwa jijini Dar akiwamo Sadalla Lipangile aliye majeruhi.

Msafara huo unatarajiwa kuwasili Mwadui, Jumamosi na itapumzika kabla ya kujifua mazoezi na kushuka uwanjani Jumatatu, huku wakiwa na matumaini makubwa ya kuendeleza ushindi.

Mara baada ya mechi hiyo ya Jumatatu, KMC watasafiri hadi Bukoba, kuvaana na wenyeji wao Kagera Sugar katikam pambano litakalochezwa Septemba 25 kwenye Uwanja wa Kaitaba.